Ivo Mapunda : Mkiniiga Staili ya Kitaulo..Naingia na Blanketi Kabisa






KIPA wa Simba, Ivo Mapunda huwa haishiwi vituko jamani, eti kwa sababu idadi ya makipa wanaobeba mataulo Ligi Kuu Bara imekuwa ikiongezeka, amesema kama watakuwa wengi, atabadilisha staili hiyo na sasa ataingia na blanketi uwanjani.

Ivo amekuwa kivutio kwenye mechi kutokana na staili yake hiyo ya kuingia na taulo uwanjani. Ni staili ambayo ilimpa umaarufu tangu alipokuwa anaichezea Gor Mahia ya Kenya japo imekuwa ikihusishwa na imani za kishirikina.

Akizungumza na Mwanaspoti, Ivo alisema: “Hii staili ya taulo naipenda, lakini kwa sasa naona wanaobeba wamekuwa wengi, kama wataendelea kuzidi nitaibadilisha.

“Na kama nitabadili, badala ya taulo, sasa nitakuwa naingia uwanjani na blanketi, nikiwa na mwonekano mwingine.”

Kutokana na taulo hilo, amekuwa akiingia kwenye migogoro na wachezaji wa timu pinzani pamoja na waamuzi.

Ugomvi wao ni pale anapokuwa anataka kulitundika kwenye nyavu za goli, jambo ambalo wenyewe wanaona siyo sahihi na kumtaka aliweke chini na wanafikiri kuwa upo uchawi ingawa mwenyewe huwa anapinga suala hilo.