Blind nje wiki sita, Man United hoi

Balaa Daley Blind, anaweza kuwa nje hadi wiki sita baada ya kuumia vibaya goti lake akiwa katika majukumu ya timu ya taifa lake la Uholanzi juzi Jumapili. 
In Summary
Kiungo mkabaji mahiri wa United, Daley Blind, anaweza kuwa nje hadi wiki sita baada ya kuumia vibaya goti lake akiwa katika majukumu ya timu ya taifa lake la Uholanzi juzi Jumapili katika pambano dhidi ya Latvia waliloshinda mabao 6-0.
SHARE THIS STORY
BUNDI amegoma kuondoka katika paa la Old Trafford. Wakati kikosi cha Manchester United kikiwa katika majanga ya kupoteza pointi hovyo, ndio kwanza timu hiyo inakumbwa na majeruhi zaidi
Kiungo mkabaji mahiri wa United, Daley Blind, anaweza kuwa nje hadi wiki sita baada ya kuumia vibaya goti lake akiwa katika majukumu ya timu ya taifa lake la Uholanzi juzi Jumapili katika pambano dhidi ya Latvia waliloshinda mabao 6-0.
Blind alianguka katika dakika ya 19 kwenye Uwanja wa Amsterdam Arena na kukanyagwa na mchezaji wa Latvia, Eduards Visnakovs. Huyo ni mchezaji wa 39 kupata majeruhi katika kikosi cha Louis van Gaal tangu alipochukua nafasi klabuni hapo Julai mwaka huu. Pia ni wastani wa mchezaji mmoja kuumia kila baada ya siku tatu.
Blind aliweza kuondoka uwanjani akitembea mwenyewe, lakini imedaiwa kuwa atakuwa nje kwa wiki nne hadi sita. Ingawa vipimo vilitarajiwa kujulikana jana Jumatatu jioni, lakini inadaiwa kuwa Blind atakuwa nje mpaka Mwaka Mpya.
Blind alitumia mtandao wake wa Instagram kuthibitisha majeraha hayo akisema: “Najivunia kucheza mechi 25 za timu ya taifa ya Uholanzi, lakini nimejisikia vibaya kutokana na majeraha haya.”
Naye kocha wa sasa Uholanzi, Gus Hiddink, alisema: “Mimi si daktari, lakini nina mtazamo hasi. Goti lake lilikunjika na inawezekana kuna madhara makubwa. Kesho (jana Jumatatu) kutakuwa na vipimo maalumu.”
Huo ni mwendelezo wa wachezaji majeruhi katika kikosi cha United ambacho tayari kinatazamiwa kuwakosa wachezaji muhimu katika mechi zijazo.
Kipa namba moja, David De Gea, atakuwa nje kwa wiki nne baada ya kuumia kidole akiwa na Hispania Ijumaa iliyopita.
Mabeki wanne wa United wana matatizo. Wakati Phil Jones akiwa ameumia ugoko, Muargentina Marcos Rojo ameteguka bega, Rafael Da Silva ana matatizo ya misuli wakati Jonny Evans ameumia kifundo cha mguu.
Wiki iliyopita, kiungo Michael Carrick alijitoa katika kikosi cha timu ya taifa ya England kutokana na tatizo la nyonga wakati Ander Herrera amekuwa na tatizo la ufa katika mbavu.
Mshambuliaji, Radamel Falcao, amekuwa na tatizo la kiazi cha mguu na anafanyishwa mazoezi maalumu kwa ajili ya kucheza pambano dhidi ya Arsenal Jumamosi.