KAFULILA AZIDI KUKOMAA NA ESCROW

Dar es Salaam. Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila amesema atawasilisha bungeni hoja binafsi ya kutokuwa na imani na Serikali, iwapo ripoti za uchunguzi wa mabilioni ya fedha za Escrow zilizotochotwa kifisadi haitajadiliwa Bunge lijalo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Kafulila (NCCR Mageuzi) alisema amechukua uamuzi huo kutokana na ubabaishaji wa makusudi kuiweka wazi ripoti hiyo. “Nasisitiza kwamba fedha za Escrow, Dola za Marekani 270 milioni, zimetolewa kifisadi na ndio sababu kwa muda sasa umekuwapo mkakati wa kuzuia ripoti za uchunguzi zisijadiliwe Bunge lijalo. Wito wangu kwa Serikali, iwapo ripoti hii haitaletwa, Bunge lijalo halitakalika. Nitapeleka hoja ya kutokuwa na imani na Serikali,” alisema.
Alisema ni wazi Kampuni ya Ufuaji Umeme ya IPTL na ya Pan African Power Solution (PAP), zimejipanga kuwapotosha Watanzania wasijadili masuala ya biashara ndani ya IPTL, wakati mauziano yao yana utata wenye masilahi ya Taifa kwa kuwa yanaambatana na kodi, hasa kitendo cha kuripoti kuwa asilimia 70 za hisa za IPTL ziliuzwa kwa Sh6 milioni, ikimaanisha ukwepaji mkubwa wa kodi.
“Ninasisitiza, Singasinga Sethi (Singh Sethi, Mkurugenzi wa Pan Africa Power Limited) aache kampeni za kupotosha umma wa Watanzania kwa nguvu ya fedha.
“Mkakati unaoendelea kuhakikisha ripoti haziji Bunge lijalo, usitishwe mara moja kwa sababu nchi inaumia, hakika sitakubali agenda niliyoanzisha ihujumiwe,” alisema.
Aliwahakikishia Watanzania kuwa katika suala hilo lazima ‘vigogo’ waliohusika waondolewe. SOURCE>> Mwananchi