SAKATA LA DK. SLAA KUTAKA KUUAWA LAZIDI KUPAMBA MOTO---->>




Lile sakata linaloendelea kutingisha katika siasa za Tanzania, la aliyekuwa mlinzi wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Dk. Wilbroad Slaa aitwaye Khalid Kangezi, kudaiwa kushirikiana na baadhi ya wanachama wa CCM, akiwemo makamu mwenyekiti wake (Bara), Philip Mangula na maafisa wa usalama wa taifa (TISS) kupanga njama za kumuua kiongozi huyo, linazidi kuchukua sura mpya.
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Dk. Wilbroad Slaa.
MAELEZO YA AWALI
Katika maelezo ya awali yaliyotolewa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Mabere Marando, ilielezwa kuwa chama hicho kilikuwa kikimfuatilia mlinzi huyo kwa kipindi kirefu baada ya kuhisi kwamba anashirikiana na viongozi wa CCM na maafisa usalama kutaka kukatisha uhai wa Dk. Slaa kwa kumuwekea sumu kwenye chakula au kinywaji.
“Kangezi kwa miaka miwili tumebaini amekuwa akitumika kuvujisha taarifa za Chadema. Amekiri hilo kwa maandishi na kutaja namba za watu wote wa usalama wa taifa aliokuwa akiwapelekea taarifa hizo,” alisema Marando na kuendelea kutoa ufafanuzi wa jinsi mlinzi huyo alivyokuwa akivujisha siri mpaka walipomnasa.
Katika maelezo hayo, Marando alieleza kuwa wameamua kumfikisha mlinzi huyo polisi kwani alichokuwa anakifanya, lilikuwa ni kosa la jinai.
KANGEZI AKANUSHA, AIBUA MAPYA
Siku chache baadaye, Kangezi aliitisha mkutano na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Habari Maelezo, Posta jijini Dar es Salaam na kukanusha vikali tuhuma hizo na kuibua mambo mengine mapya.
Akaeleza kwamba hajawahi kuwa na mpango huo isipokuwa yeye ndiye aliyenusurika kifo baada ya kufungiwa chumbani kwa zaidi ya saa sita na viongozi wa chama hicho wakiwa wanamsulubu akiwa uchi wa mnyama.
Aliyekuwa mlinzi wa Dk. Slaa Khalid Kangezi.
Kangezi alisema alifanyiwa hivyo akishinikizwa asaini karatasi ya maelezo kuwa ana njama za kutaka kumpa sumu Dk. Slaa akishirikiana na watu wengine ambapo kutokana na kutishiwa maisha, alikubali kusaini kwani ndani ya chumba alichokuwa anateswa, kulikuwa na begi lenye visu ambavyo anadai vilitaka kutumiwa kumuua.
MARANDO AZUNGUMZA NA UWAZI MIZENGWE
Baada ya kupata taarifa juu ya kilichozungumzwa na Kangezi kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, Uwazi Mizengwe lilimtafuta tena Marando ambapo alikuwa na haya ya kuzungumza:
“Hilo suala lipo polisi, huyo Kangezi tulimkabidhi kwa polisi kama nilivyosema awali kwa sababu alichokuwa anakifanya lilikuwa ni kosa la jinai.
Kama wao polisi wamemuona hana hatia au wameshindwa kufanyia upelelezi tulichowaambia, sisi hatuwezi kusema chochote, hata wakitaka wamuachie ni juu yao.
“Hatuwezi kuendelea kubishana na mlinzi, sisi tuseme hivi, yeye aseme vile kisha tuendelee kubishana, hatuwezi kufanya hivyo. Tulichokisema awali ndicho hichohicho, iliyobaki ni kazi ya polisi,” alisema Marando.