Na ninasema hivi hasa kutokana na ukweli ambao nafsi zote mbili zinakubaliana kuwa mwanaume ndiye kichwa cha nyumba. Usemi huu unaweza kuonekana ni mwepesi kama utaangaliwa kwa upande mmoja tu, ambao kimsingi unabeba maana ya uwajibikaji juu ya majukumu ya kuilea na kuilinda familia.
Na unapozungumzia kuhusu jambo hili, akili ya kawaida na haraka, ni juu ya wajibu wa mume au baba katika kuhakikisha familia inapata huduma zote muhimu kama chakula, malazi, matibabu, masomo na kadhalika.
Ni kweli. Lakini maana halisi ya kichwa cha nyumba ni kuwa huyu ndiye kila kitu. Wote tunajua, binadamu anaweza kukosa mikono na miguu, lakini akaendelea kuitwa mtu kwa sababu tu, anacho kichwa. Bila kichwa, kiumbe hicho kitaitwa jina lingine lisilo binadamu.
Uzoefu unaonyesha, uharibifu wa ndoa au uhusiano mwingi wa kimapenzi, huanza kupata msukosuko baada ya baba kuanza kutoka nje ya mstari. Nje ya mstari hakumaanishi kushiriki mapenzi, bali hata kuacha kutekeleza baadhi ya majukumu yake. Baba, kwa sababu zozote, anapozembea au kukataa kulipa ada ya mtoto, ni wazi kuwa atamfanya mama kuanza kuwaza mambo mengi hata yaliyo nje ya uwezo wake.
Hii ni kauli ambayo hakuna yeyote angependa kuisikia, lakini kwa kuwa kulikuwa na mazungumzo yaliyotangulia, ni wazi kuwa kitu kikubwa kinachotakiwa ili kuondoa mzozo, ni busara. Kama mnunaji ni mama, ni rahisi baba kumbembeleza na pengine kwa kutumia mamlaka yake, anaweza kulipooza jambo hilo.
Lakini naona kabisa jinsi gani suala hilo linaweza kuwa kubwa kama baba ndiye atavimba mashavu kwa hasira baada ya kauli kama hii. Na labda ieleweke kuwa siyo nia yangu kutetea nafasi ya mwanaume katika uhusiano wa kimapenzi, lakini kama tunataka mambo yetu kwenda sawa, daima lazima tuwe tayari kukubaliana na ukweli, hata kama unatuumiza.
Kwa hiyo, nimalizie tu kwa kuwasihi wababa, kama wenyewe hawawezi kusoma hapa na kuelewa ujumbe ninaowatumia, basi akina mama waonyesheni hapa wasome, kwamba wao ndiyo wenye nafasi kubwa ya kulilea na kulienzi penzi tulilomo!