KOCHA Mkuu wa Simba Partick Phiri amefanya uamuzi mgumu katika kikosi chake kwa kumweka benchi nahodha na beki mzoefu wa timu Joseph Owino kwenye mechi dhidi ya Stand na sasa amesisitiza lazima akae kikao na mchezaji mmoja baada ya mwingine.
Akizungumza na Mwanaspoti akiwa na machungu ya
matokeo ya sare yanayoikumbuka timu yake Phiri alisema kwa sasa ni wazi
kwamba anafanya kazi katika mazingira magumu ya kuwa na presha ambapo
hajajua kiini cha tatizo linaloimaliza timu yake.
Phiri amepanga kuwapa wachezaji mapumziko ya siku
mbili na mara baada ya kurudi kambini anataka kufanya kikao tofauti na
kila mchezaji na wasaidizi wake kwa nyakati tofauti.
Alisema kuanzia keshokutwa Jumatano timu yake
itakuwa na wiki mbili nzito za kujiimarisha kwa maandalizi ya nguvu
kujiweka sawa kabla ya kuwavaa wapinzani wao wa jadi Yanga ambao
ametamka kwamba wanazidi kuimarika kadri ya siku zinavyosonga huku wao
wakidhoofika.
“Simba ni timu kubwa haiwezi kuzoea hali hii, siyo
heshima yake, nimekaa hapa kwa muda mrefu katika nyakati tofauti lakini
hali hii haijawahi kunitokea na mpaka sasa sijaelewa nini kiini cha
haya matokeo ambayo yanamuumiza kila mmoja anayeipenda timu hii,”alisema
Phiri.
“Ukiangalia mazoezi yetu wachezaji wanajituma kwa
hali ya juu sana lakini unapokuja kwenye mechi hali inakuwa mbaya sana,
tunafunga goli lakini linarudi kwa haraka sana ni lazima nikutane na
mchezaji mmoja mmoja na wasaidizi wangu pia kila mmoja kwa wakati wake
tusaidiane kujua tunakosa wapi.
“Hatuwezi kucheza na Yanga tukiwa katika hali hii
ni lazima tujipange vyema ukiwaangalia Yanga utagundua kwamba ni timu
inayoimarika kila wanapoamka huku sisi tukinyong’onyea. Lazima tuamke
tutakuwa na wiki mbili ngumu kabla ya mchezo huo,”alisisitiza Phiri.
